Biblia ni kitabu cha ajabu kuliko vitabu vyote duniani. Kwa nini? Ni kwa sababu jina lenyewe lina maana ya vitabu au maktaba ya Mungu, yenye jumla ya vitabu sitini na sita. Tena, Biblia ina waandishi wapatao arobaini, waliotumiwa na Mungu kuiandika Biblia kwa vipindi tofauti, kati ya muda wa miaka 1500 na 1600, wakiongozwa na Mungu mwenyewe, hivyo kuifanya Biblia iwe na mwandishi mmoja tu, yaani Mungu.

Jambo lingine la ajabu, Mungu aliwatumia waandishi wa fani mbalimbali, mazingira na nyakati tofauti wakiwemo manabii, wafalme, wakulima, wafugaji, wavuvi, watoza ushuru, madaktari, wajenzi n. k; hata hivyo Biblia imekuwa na umoja wa ajabu, bila kuhitilafiana kunakotokana na mazingira wala nyakati. Umoja huu unatuthibitishia kuwa mwandishi wa Biblia ni mmoja, ambaye amekuwako nyakati zote za historia ya dunia, yaani Mungu.

“Maana unabii haukuletwa popote kwa mapenzi ya mwanadamu; bali wanadamu walinena yaliyotoka kwa Mungu, wakiongozwa na Roho Mtakatifu(2Pet. 2:21).

Mungu ndiye Alfa na Omega, yaani mwanzo na mwisho, (Uf. 1:17); “Aliyeko na aliyekuwako na atakayekuja (Uf.4:4), “Niko ambaye Niko” Kut.3:14; Yoh. 8:58. Huyu ndiye aliyewapa waandishi maneno ya kuandika katika vizazi vyote. Jambo lingine la ajabu kuhusu kitabu hiki ni kwamba, ni kitabu peke ambacho kimeenea duniani pote na kusomwa na watu wengi. Pia ni kitabu kilichowatenganisha watu na kuwafarakanisha kuliko kitabu kingine chochote duniani; lakini wakati uo huo ni kitabu chenye majibu ya maswali mengi ya wanadamu duniani kuliko kitabu kingine chochote.

Ili kuielewa Biblia vema, ni sharti kutumia kanuni ambazo zitalinda umoja wa Biblia na kuleta maana zisizohitilafiana na kupingana. Masomo muhimu yote duniani kama vile sayansi au hisabati na mengineyo, yanafundishwa kwa kutumia kanuni maalumu ili kutunza usahihi wake; vinginevyo kila mmoja angekuwa na majibu yake tofauti na mwingine. Kwa kuwa tunajua kuwa Biblia ni somo muhimu sana kuliko masomo yote duniani, sharti isomwe na kufasiriwa kwa kanuni maalumu ili kulinda umoja wake, na kuepuka athari za kupoteza maana halisi ya Mungu iliyokusudiwa; huku tukitumia akili zetu za kibinadamu. Kuna mitafaruku mingi sana tunapoingia katika masuala ya imani, inayosababishwa na mafundisho yasiyozingatia kanuni za kusoma na kufasiri maandiko ya Biblia. Mungu ni mwaminifu kutoa ufunuo kwa njia ya Roho kuhusu Neno lake (Yoh.6:63; 1Kor.2:13,16). Lakini kwa kuwa ufunuo ni suala la kiroho na siri kati ya mwanadamu na Mungu wake, hakuna mtu mwingine wa pembeni awezaye kujua kinachoendelea. Hii imekuwa sababu ya watu wengi kudai kwamba wamefunuliwa na Mungu wakati ni mawazo yao wenyewe. Ili kuepuka athari hizi, Mungu ametupa kanuni zake ambazo zinaweza kumsaidia mtu yeyote hata yule asiyejua mambo ya ufunuo wa Roho; kwa sababu kanuni ni kanuni, haijalishi umeokoka au la! Kama ilivyo kwa masuala mengine yoyote yanayohitaji kutekelezwa kwa kutumia kanuni, haijalishi kuwa unaamini au la, kanuni itafanya kazi yake!

Hebu nitumie mifano michache ya hesabu za kujumlisha na kuzidisha zenye tarakimu mbili: 25+25, ukijumlisha kuanzia kushoto kwenda kulia, jawabu lake litakuwa 410; lakini ukijumlisha kuanzia kulia kwenda kushoto, jawabu lake litakuwa 50. Majawabu yote mawili ni sahihi iwapo hakuna kanuni ya hisabati ya kujumlisha. Hakuna mmoja kati ya hawa wawili atakayekuwa na ujasiri wa kumkosoa mwenzake kuwa amekosea iwapo hakuna kanuni inayomhakikishia yeye kuwa yuko sahihi. Lakini kwa kuwa kanuni ya hesabu hii ni kujumlisha kutoka kulia kwenda kushoto, basi atakuwa na uhakika kuwa jawabu sahihi ni 50. Uhakika wa jibu hili unatokana na kanuni ya hesabu za kujumlisha!

Mfano mwingine: Unapotaka kuhakikisha usahihi wa hesabu ya kuzidisha, ni sharti kugawa jawabu na tarakimu mojawapo kati ya mbili zilizotumika kuzidisha, kwa mfano, 6 x 8= 48; na 48 ukigawa kwa 8, jawabu litakuwa 6; hapo unakuwa na uhakika wa jawabu lako kuwa ni sahihi. Kwa hiyo, bila kuwa na kanuni ya kuhakikisha usahihi wa jawabu lako, huwezi kujua kama uko sahihi au la. Kutokana na mifano hii miwili, tunaona jinsi ilivyo muhimu kusoma na kuifasiri Biblia kwa kutumia kanuni zake, ili kuwa na uhakika wa yale tunayoyasoma na kuyafundisha, tusifundishe upotofu. “Kila Neno la Mungu limehakikishwa; yeye ni ngao ya wamwaminio. Usiongeze neno katika maneno yake; asije akakulaumu, ukaonekana u mwongo” (Mith.30:5,6).

Je, tutazipata wapi kanuni za kutuwezesha kusoma na kufasiri Biblia? Jibu la swali hili ni rahisi kwa sababu, kanuni hizi zinapatikana katika kitabu hiki cha ajabu, yaani Biblia. Kwa hiyo, haifai mtu fulani kuinuka na kutoa maana ya maandiko matakatifu kwa kutumia mawazo na akili zake; au kwa kusema, “nadhani, huenda, bila shaka” au kutumia misimamo ya dini, au mkuu fulani katika dini, au imani ya madhehebu kwa kusema, “dini yetu inasema hivi” badala ya kutumia msimamo wa mwandishi mkuu wa Biblia ambaye ni Mungu. “Mkijua neno hili kwanza, ya kwamba hakuna unabii katika maandiko upatao kufasiriwa kama apendavyo mtu fulani tu” (2Pet.1:2).

Yesu alitusaidia sana kutupa mwongozo wa kuielewa Biblia na makusudi yake aliposema, “Msidhani ya kuwa nalikuja kuitangua torati au manabii la, sikuja kutangua, bali kutimiliza. Kwa maana, amin, nawaambia, mpaka mbingu na nchi zitakapoondoka, yodi moja wala nukta moja ya torati haitaondoka, hata yote yatimie” (Math.5:17,18).

“…..Hayo ndiyo maneno yangu niliyowaambia nilipokuwa nikali pamoja nanyi, ya kwamba ni lazima yatimizwe yote niliyoandikiwa katika torati ya Musa, na katika manabii na Zaburi. Ndipo akawafunulia akili zao wapate kuelewa na maandiko” (Luka 24:44,45).

“Mwayachunguza maandiko, kwasababu mnadhani kwamba ninyi mna uzima wa milele ndani yake; na hayo ndiyo yanayonishuhudia. Kwasababu kama mngemwamini Musa, mngeniamini mimi; kwa sababu yeye aliandika habari zangu. Lakini msipoyaamini maandiko yake, mtayaamini wapi maneno yangu?” (Yoh.5:39, 46, 47).

“…..Akiwaonya mambo yake Yesu, kwa maneno ya sheria ya Musa na ya manabii, tangu asubuhi hata jioni. Wengine waliamini yale yaliyonenwa, wengine hawakuyaamini” (Mdo 28:23, 24).

Katika maandiko yote haya hapa juu, tunaupata ukweli ufuatao:

 1. Torati, Zaburi na Manabii, ziliandikwa kwa ajili ya Yesu.

 2. Yesu alikuja kuyatimiza yote aliyoandikiwa katika Torati, Zaburi na Manabii.

 3. Yote yaliyoandikwa yataendelea kutimizwa mpaka hapo mbingu na nchi zitakapoondoka (kuja kwa Yesu mara ya pili)

 4. Wanafunzi wake hawakuijua siri hii mpaka walipofunuliwa akili zao na Yesu, baada ya kufufuka kwake.

Hapa tunaona kuwa, Agano la kale limekuwa kama ramani ya nyumba iliyochorwa; Agano jipya linajenga mpango wa Mungu kwa kufuata ramani iliyochorwa na Mungu mwenyewe katika Agano la kale, kama fundi stadi. Fundi washi anahitaji kujua jinsi ya kuisoma ramani vema, ili kujenga nyumba kama ilivyokusudiwa na mchoraji bila kupoteza vipimo au sura ya nyumba. Mitume, manabii, wainjilisti, wachungaji na waalimu, hao wote ni wajenzi wa kanisa la Mungu. “Maana msingi mwingine hakuna mtu awezaye kuuweka, isipokuwa ni ule uliokwisha kuwekwa, yaani Yesu Kristo” (1Kor.3:11). Hatuwezi kujenga kwa kutumia mafundisho ambayo Yesu hakutuachia sisi, tukiwa ndio kanisa lake; naye ndiye mtimizaji wa Torati, Zaburi na Manabii; tutakuwa sawa na fundi washi anayeacha kuisoma ramani aliyopewa na kuanza kuchora ramani yake. Pia ikumbukwe kwamba, hata katika mazingira yetu, kuna wajenzi wengi wa nyumba za kawaida, wasio na uwezo wa kusoma ramani iliyochorwa, ingawa wanaweza kujenga bila kutumia ramani.

Yesu alisema, “Torati na manabii vilikuwepo mpaka Yohana; tangu wakati huo, habari njema ya ufalme wa Mungu hutangazwa, na kila mtu hujiingiza kwa nguvu” (Luka 16:16).

Alisema tena, “Kwa maana Manabii wote na Torati walitabiri mpaka wakati wa Yohana” (Math. 11:13). Katika maandiko haya mawili tunaona kuwa Torati yote na Manabii wote, ujumbe wao ulilenga kufikia wakati wa Yohana mbatizaji, ambao pia ulikuwa ni wakati wa Yesu mwenyewe duniani; lakini baada ya muda huo kupita, unaobaki ni muda wa utekelezaji wa yale yote yaliyoandikwa katka Agano la kale. Yesu alitekeleza yale yaliyomhusu kwa wakati wake; yaliyosalia yalitekelezwa na mitume; baada ya hapo, kanisa limeendelea kutekeleza yote yaliyobaki na kulihusu, litaendelea na kazi hiyo mpaka wakati wa kuja Yesu mara ya pili, yaani mwisho wa dunia. Yohana alikuwa ndio mwisho wa unabii; hakuna unabii mwingine uliotolewa baada ya Yohana mbatizaji, isipokuwa Injili za Yesu, nyaraka za mitume na ufunuo, ambamo ndani yake tunapata ufafanuzi au kuisoma ramani ya Agano la kale, iliyochorwa kuishia mwisho wa dahari, yaani kuja kwa Yesu mara ya pili, au mwisho wa dunia. Kwa maneno mengine ni kusema kwamba, hakuna ramani nyingine iliyochorwa au itakayochorwa baada ya Yohana mbatizaji, bali ni ujenzi utakaoendelea. Zaidi ya hayo ni kusema kuwa, hata kitabu cha ufunuo wa Yohana hakileti jambo lolote lililo jipya, ambalo halikunenwa na Torati, Zaburi, Manabii, Yesu na mitume. “…..Na juu ya mwamba huu nitalijenga kanisa langu; wala milango ya kuzimu haitalishinda” (Math.16:18).

Agano la kale lina sehemu kuu tatu ambazo ni Torati, Zaburi na Manabii; pia Agano jipya lina sehemu kuu tatu zinazofafanua Agano la kale, nazo ni Injili, Nyaraka na Ufunuo. Ni lazima sehemu hizi zikubaliane katika maana ya kile tunachokitafuta. Kwa sababu ya umoja wa Biblia ulivyo, haifai kuitenganisha vipande vipande, hata kupoteza maana yake. Kwa kufanya kosa hilo, tutasababisha andiko moja kufasiriwa kwa maana nyingi zilizo tofauti, na kujenga mafundisho dhaifu ndani ya kanisa la Yesu Kristo, na kulifanya lishindwe kwa kushambuliwa na milango ya kuzimu. Yesu alirehemu kanisa lake!

Msomaji anapoijua siri ya umoja wa Biblia, na jinsi ambavyo haiwezi kutofautiana kutoka andiko hata andiko; au mwandishi na mwandishi; au karne na karne; maana mwandishi mkuu ni mmoja yule yule. Kujua huku kutamsaidia msomaji kutokuielewa vibaya Biblia, au kupata maana ambayo itapingana na maandiko mengine. Ukichukua kizibo cha chupa halafu ukakosea kukikalisha katika chupa, utashindwa kufunga hata ukadhani sio kizibo chake. Kama utalazimisha kufunga bila kujua kwamba umekosea kukikalisha inavyotakiwa, hatimaye hata wakati wa kufungua unaweza kushindwa, na ukalazimika kukivunja. Tatizo si la kizibo, tatizo ni la mfungaji ambaye hakujua jinsi ya kukikalisha inanyotakiwa. Vivyo hivyo, ndivyo ilivyo katika Neno la Mungu! Wasomaji wengi wanadhani kuwa Biblia ni ngumu sana kuielewa; ingawa kuna ukweli katika jambo hili, kwa sababu yatambulikana kwa jinsi ya roho; lakini tatizo kubwa ni kwamba mtu anaisoma Biblia huku akiwa ametanguliza mawazo binafsi na mapokeo ya kidini, hivyo kushindwa kuiunganisha ili kuipata maana iliyo sahihi.

Wayahudi waliyajua sana maandiko ya torati na kujisifu katika jambo hilo; lakini Yesu alipokuja walishindwa kuyaunganisha maneno ya torati na ya Yesu, wakiyafanya kuwa ni vitu viwili tofauti, na kushindwa kabisa kumwelewa Yesu ni nani. Walidai kumjua Yesu, lakini walimkataa Yesu alipojiita kuwa ni Mungu. Mifano: Kumb.8:3 na Math.4:4; Isa.6:9,10 na Math.13:14,15; Kumb.18:15 na Yoh.5:47; Zab.82:6 na Yoh.10:34; Yoeli 2:28,29 na Mdo 2:16-21; Zab.16:8-11 na Mdo 2:25-28; Zab.110:1 na Luka 20;41-44; Luka 24:44-46. Haya ni baadhi ya maandiko machache ambayo Yesu aliwakumbusha Wayahudi kwamba, yale waliyokuwa wakiyasoma katika Torati, Zaburi na Manabii, yalimhusu yeye na wasingeweza kumtenganisha na maandiko hayo. Kwa hiyo, waliosoma agano la kale bila kumwona Yesu, na wale waliomwona na kumsikia, na sisi tunaosoma sasa, hakuna tofauti yoyote. Paulo katika waraka wake anasema, “Hata imekuwa, sisi tangu sasa hatumjui mtu awaye yote kwa jinsi ya mwili. Ingawa sisi tumemtambua Kristo kwa jinsi ya mwili, lakini hatumtambui hivi tena” (2Kor.5:16).

Mtume Yohana naye katika waraka wake anasema, “Lile lililokuwako tangu mwanzo, tulilolisikia, tuliloliona kwa macho yetu, tulilolitazama, na mikono yetu ikalipapasa, kwa habari ya Neno la uzima; na uzima huo ulidhihirika, nasi tumeona, tena twashuhudia, na kuwahubiri ninyi ule uzima wa milele, uliokuwa kwa Baba, ukadhihirika kwetu. Hilo tuliloliona na kulisikia, twawahubiri na ninyi; ili nanyi pia mpate kushirikiana nasi; na ushirika wetu ni pamoja na Baba , na pamoja na Mwana wake Yesu Kristo” (1Yoh.1:1-3).

Mtume Petro naye anasema, “Naye mwampenda, ijapokuwa hamkumwona; ambaye ijapokuwa hamwoni sasa, mnamwamini; na kufurahi sana, kwa furaha isiyoneneka, yenye utukufu….Wakafunuliwa ya kuwa si kwa ajili yao wenyewe, bali kwa ajili yenu walihudumu katika mambo hayo, ambayo sasa yamehubiriwa kwenu na wale waliowahubiri ninyi Injili kwa Roho Mtakatifu aliyetumwa kutoka mbinguni. Mambo hayo malaika wanatamani kuyachungulia.” (1Pet.1:8,12).

Mwandishi wa kitabu cha Waebrania anaandika kwa kusema, “Mungu ambaye alisema zamani na baba zetu katika manabii kwa sehemu nyingi na kwa njia nyingi, mwisho wa siku hizi amesema na sisi katika mwana , aliyemweka kuwa mrithi wa yote, tena kwa yeye aliufanya ulimwengu” (Ebr.1:1).

“Na watu hao wote wakiisha kushuhudiwa kwa sababu ya imani yao, hawakuipokea ahadi; kwa kuwa Mungu alikuwa ametangulia kutuwekea sisi kitu kilicho bora, ili wao wasikamilishwe pasipo sisi” (Ebr.11:39,40).

Waandishi hawa wote wanakiri jambo moja lile lile kwamba, hakuna tofauti kati ya watu walioisikia torati ya Musa, zaburi, manabii na wale waliomsikia Yesu ana kwa ana na kumwona; pia na sisi tuliomwamini bila kumwona kwa jinsi ya mwili. Sisi sote tumelipokea neno lile lile lililo sawa kwa njia ya imani iliyo katika Kristo Yesu. Mungu wetu hawezi kubadilika-badilika katika maneno yake; ni yeye yule, jana na leo na hata milele. Huu ndio umoja wa Biblia ulio imara na hauwezi kuyumbishwa na mwanadamu yeyote. Mtume Paulo aliwaonya wakristo wa Kolosai kuhusu mchanganyo huu wa mafundisho yanayoingizwa kwa ujanja wa watu kwa kusema, “Angalieni mtu asiwafanye mateka kwa elimu yake ya bure na madanganyo matupu, kwa jinsi ya mapokeo ya wanadamu, kwa jinsi ya mafundisho ya awali ya ulimwengu, wala si kwa jinsi ya Kristo” (Kol.2:8).

Mungu amekuwa akijifunua kwa watu wake kwa njia tofauti-tofauti kulingana na majira na wakati; lakini akiwa ni yeye yule. Alijidhihirisha kwa watu wa kale kama Mungu Baba, Mwenyezi, Yehova, Niko ambaye niko, Muumba wa mbingu na nchi, Mungu wa Ibrahimu, Isaka na Yakobo, Baba wa milele, na mengine mengi; lakini zamani hizi amejidhihirisha kama Mwana, na majina hayo yote pia ni yake, kuonyesha kwamba ni Mungu yeye yule. Alifanya agano la kale, zamani hizi amefanya agano jipya, lakini Mungu ni yeye yule. Kwa hiyo maagano haya mawili hayapingani, bali kila moja linaleta tafsiri nzuri kwa lingine. Ili kulielewa vema agano la kale, unahitaji kulielewa agano jipya; kadhalika, ili kulielewa vema agano jipya, unahitajika kulielewa vema agano la kale, kwa kuwa mwandishi wa maagano haya ni yule yule mmoja.

Somo letu litaendelea wakati mwingine……………………

Usisahahu kufollower, comment, like na kushare kwa wapendwa wengine.

Source: Mwalusambo International Ministry

Ni Mimi ndugu yako Counselor Nicholaus Simon.

Kiungo katika mwili wa kristo.

Kwa msaada ushauri au maswali

Whatsap: +255 766 635 382/+255 659 990 111

Email: pataufahamu@gmail.com/  info@mwalusambo.or.tz

  

Axact

Axact

Vestibulum bibendum felis sit amet dolor auctor molestie. In dignissim eget nibh id dapibus. Fusce et suscipit orci. Aliquam sit amet urna lorem. Duis eu imperdiet nunc, non imperdiet libero.

Post A Comment:

0 comments: