BIBLIA TAKATIFU

Tukiwa katika sehemu ya Pili ya Somo hili, NAMNA YA KUWA MTENDAJI WA NENO LA MUNGU, baada ya kujifunza katika sehemu ya kwanza umuhimu wa kuwa mtendaji wa neno,tuendelee kujifunza pamoja hapa.kusoma sehemu ya kwanza bofya hapa: http://pataufahamu.blogspot.com/2017/06/namna-ya-kuwa-mtendaji-wa-neno-la-mungu.html


KUWA MTENDAJI WA MUNGU NI SAWA NA KUITEKA NCHI YA AHADI
" Ikawa baada ya kufa kwake Musa, mtumishi wa Bwana, Bwana akamwambia Yoshua, mwana wa Nuni, mtumishi wa Musa, akasema, Musa mtumishi wangu amekufa, haya basi,ondoka, vuka mto huu wa Yordani; wewe na watu hawa wote, mkaende hata nchi niwapayo wana wa Israeli. Kila mahali zitakapokanyaga nyayo za miguu yenu, nimewapa ninyi, kama nilivyomwapia Musa. Tangu jangwa hili na mlima huu,….. Hapatakuwa mtu ye yote atakayeweza kusimama mbele yako siku zote za maisha yako; kama nilivyokuwa pamoja na Musa, ndivyo nitavyokuwa pamoja na wewe; sitakupungukia wala sitakuacha. Uwe hodari na moyo wa ushujaa, maana ni wewe utakayewarithisha watu hawa nchi hii niliyowaapia baba zao ya kwamba nitawapa."
 (Yoshua 1:1-6)

Haya ni baadhi tu ya maagizo ambayo Bwana alikuwa anamweleza Yoshua, mwana wa Nuni, juu ya kuwaongoza wana wa Israeli kwenda kaanani. Hii ilikuwa mara tu baada ya Musa kufa.

Ni budi ufahamu ya kuwa kusudi la Mungu, kuwatoa wana wa Israeli toka nchi ya Misri, lilikuwa si tu kuwatoa toka katika utumwa.

Kusudi la Mungu kuwaondoa wana wa Israeli toka Misri lilikuwa ni kuwatoa katika utumwa, na kuhakikisha Yeye mwenyewe amewafikisha katika nchi ya Kanaani, iliyokuwa ni nchi ya ahadi.

Safari ya wana wa Israeli toka Misri hadi katika nchi ya ahadi, tunaweza kuifananisha na maisha ya kiroho ya kanisa, au tuseme maisha ya kikristo.

Yesu Kristo alikufa msalabani na kufufuka si tu ili atuondoe toka katika ufalme wa Ibilisi na kazi zake – mauti, dhambi, magonjwa na umaskini.

Kusudi la Kristo kufa msalabani na kufufuka lilikuwa ni kutuhamisha toka chini ya ufalme wa shetani na kazi zake na kuhakikisha yeye mwenyewe kuwa anatuingiza katika ufalme wa Mungu na kurithi vitu vyote vilivyomo (Wakolosai 1:13,14)

Mungu tunayemtumikia sasa, ni yeye yule ambaye pia alisema na Musa na Yoshua.

Maagizo aliyopewa Yoshua, ni maagizo ambayo pia yametolewa kwetu sisi kama wakristo. Tofauti
iliyopo ni kwamba utekelezaji wake wa wakati wa Joshua ulikuwa wa kimwili, wakati sasa hivi (tangu kanisa lizaliwe) tunayatekeleza maagizo hayo hayo katika roho.

Maagizo haya yanafanana sana na hali ambayo ipo katika kanisa sasa, katika maisha ya watu wa Mungu. Lakini kabla hatujalijadili hili; na tuyatafakari maagizo ya Bwana kwa Yoshua.

Ukisoma historia ya wana wa Israeli, utaona ya kuwa, walikaa Misri katika hali ya utumwa kwa muda wa miaka mia nne.

Kwa sababu ya mateso makubwa waliyokuwa wanapata, walikuwa wakimlilia Mungu wao usiku na mchana. Siku moja Musa alipokuwa akichunga kundi la kondoo la Yethro mkwewe, Mungu alizungumza naye.

"Bwana akasema, Hakika nimeyaona mateso ya watu wangu walioko Misri, nami nimekisikia kilio chao kwa sababu ya wasimamizi wao; maana nayajua maumivu yao; nami nimeshuka ili niwaokoe na mikono ya wamisri, niwapandishe kutoka nchi ile, hata nchi njema, kisha pana; nchi ijaayo maziwa na asali; hata mahali pa Mkaanani, na Mhiti, na Mwamori, na Mperizi, na Mhivi, na Myebusi" (Kutoka 3:7,8).

Hiyo ndiyo nchi ambayo Bwana alikuwa anamwambia Yoshua awapeleke wana wa Israeli. Na alimwahidi jambo moja kubwa sana, nalo ni hili:

"KILA MAHALI ZITAKAPOPAKANYAGA NYAYO ZA MIGUU YENU, NIMEWAPA NINYI, kama nilivyomwapia Musa" (Yoshua 1:3)

Ingawa Bwana alikuwa amekwisha wapa wana wa Israeli nchi, na kuwatajia maeneo yenyewe na mipaka yake, bado KUMILIKI KWAO NCHI HIYO YA AHADI kulitegemea sana jinsi ambavyo wao wanachukua hatua na kuweka nyayo za miguu yao na

kutembea juu nchi hiyo.

Wasingenyanyua miguu yao na kuikanyaga nchi hiyo ya ahadi waliyopewa, wasingeweza kuimiliki nchi hiyo ya maziwa na asali.

Na kwa kuwa nchi hiyo waliyopewa ilikuwa inakaliwa na makabila mbali mbali, ni wazi kwamba kuimiliki kwao kulitegemea sana jinsi wanavyopigana vita na kushinda na kusonga mbele, hadi waikalie nchi yote ya ahadi.

Bwana alipokuwa anawaambia kuwa kila mahali zitakapokanyaga nyayo za miguu yao, amewapa wao, alikuwa ana maana kuwa kila mahali watakapopateka amewapa wao kuimiliki.

Kwa hiyo ni wazi kwamba bila kuiteka nchi hiyo kwa nguvu, wasingekula maziwa na asali walizoahidiwa na Bwana.

Je! hawa wana wa Israeli wangebaki hapo ng’ambo ya mto Yordani, bila kuchukua hatua yoyote, wangeirithi nchi ya ahadi?

Je! Joshua angewakusanya wana wa Israeli halafu awaambie waombe na kufunga ili wairithi nchi bila kuchukua hatua ingewasaidia nini?

Bwana hakuwapa maagizo ya kuiomba nchi ya ahadi, kwa sababu ALIKUWA AMEKWISHA WAPA TAYARI tangu wakati wa Ibrahimu (Mwanzo 15:8-16)

Ndiyo maana Bwana alimwambia Yoshua ONDOKA –VUKA – WEWE NA WATU HAWA WOTE, MKAENDE – NCHI NIWAPAYO WANA WA ISRAELI.

Ilikuwa ni amri yakuchukua hatua ya kuwaondoa mahali walipokuwa, na kuelekea kuimiliki nchi ya ahadi.

Bwana alipowatoa watu wake Misri, alikuwa hawaokoi na utumwa tu peke yake, bali alikuwa anawatoa utumwani ILI waweze kuirithi nchi ya maziwa na asali aliyo waahidia.

Je! umepata kitu katika mstari huu?

Tafakari wazo hili tena

Kusudi la Mungu kuwatoa wana wa Israeli toka Misri, lilikuwa si kuwatoa utumwani tu peke yake, bali pia alikuwa amekusudia kuwarithisha nchi ya ahadi, njema, iliyojaa maziwa na asali, kama alivyokuwa amemwahidi Ibrahimu alipofunga naye agano.

Na pia kusudi la Bwana kutuokoa, si tu kututoa toka katika utumwa wa dhambi, magonjwa, mauti na umaskini, bali pia ni kuturithisha nchi ya ahadi, takatifu, kama alivyokusudia tangu kuwekwa kwa misingi ya ulimwengu huu, tuwe warithi pamoja na Yesu Kristo.

Hii ni habari yenye faraja kubwa kwa watu wote wanaomtegemea Bwana. Imeandikwa hivi:

"Naye alituokoa katika nguvu za giza, akatuhamisha na kutuingiza katika ufalme wa Mwana wa Pendo lake, ambaye katika yeye tuna ukombozi, yaani, msamaha wa dhambi". (Wakolosai 1:13,14)

" Kristo alitukomboa katika laana ya torati, kwa kuwa alifanywa laana kwa ajili yetu; maana imeandikwa, Amelaaniwa kila mtu aaingikwaye juu ya mti; ili kwamba baraka ya Ibrahimu iwafikilie Mataifa katika Yesu Kristo, tupate kupokea ahadi ya Roho kwa njia ya imani". (Wagalatia 3:13,14)

Laana ya torati imeandikwa katika kumbukumbu ya torati sura ya 28:15-68. Laana hii imegawanyika katika sehemu nne kubwa; dhambi, mauti, magonjwa na umaskini. Kwa kumpokea Kristo moyoni kama Bwana na Mwokozi, mtu anakombolewa na kuondolewa chini laana hiyo.

Unaondolewa toka katika utumwa wa dhambi, unahamishwa na Kristo, na kuingizwa katika haki.

Unaondolewa toka katika utumwa wa mauti, unahamishwa na Kristo, na kuingizwa katika uzima wa milele.

Unaondolewa toka katika utumwa wa magonjwa, unahamishwa na Kristo, na kuingizwa katika uponyaji wa kutembea bila magonjwa.

Unaondolewa toka katika utumwa wa umaskini (kupungukiwa kwa vitu vya kimwili), unahamishwa na Kristo, unaingizwa katika utajiri wake usiopimika.

Nchi takatifu, ufalme wa Mungu aliye hai na haki zake zote, ni NCHI YA AHADI KWETU, tuliyopewa na Mungu katika Kristo. Ufalme wa Mungu ndiyo nchi ya ahadi kwetu.

Sisi katika Kristo ni warithi halali wa ahadi za Mungu, na tabia zake na ufalme wake.

"Kwa kuwa uweza wake wa Uungu umetukirimia vitu vyote vipasavyo uzima na utauwa, kwa kumjua yeye aliyetuita kwa utukufu wake na wema wake mwenyewe. Tena kwa hayo ametukirimia ahadi kubwa mno, za thamani, ili kwamba kwa hizo mpate kuwa washirika wa tabia ya Uungu, mkiokolewa na uharibifu uliomo duniani kwa sababu ya tamaa" (1Petro 1:3,4)

"Na kama ninyi ni wa Kristo, basi, mmekuwa uzao wa Ibrahimu, na warithi sawasawa na ahadi". (Wagalatia 3:29)

"Na kwa kuwa ninyi mmekuwa wana, Mungu alimtuma Roho wa Mwanawe mioyoni mwetu, aliaye, Aba, yaani, Baba. Kama ni hivyo, wewe si mtumwa tena bali u mwana; na kama umwana, basi u mrithi kwa Mungu" (Wagalatia 4:6,7)

Ikiwa basi tumeahidiwa mambo makubwa ya thamani namna hiyo ndani ya Kristo, mbona hali ya wakristo, hasa waliookoka imekuwa duni?

Je! tuna la kujitetea? Ni kweli tunaangamia kwa kukosa maarifa. Twapotea kwa kuwa hatuyajui maandiko wala uweza wa Mungu.

Mungu anapotuangalia anatarajia kutuona tukiishi bila kutenda dhambi kuanzia tukiwa hapa duniani. Kwa kuwa imeandikwa, "Kila mtu aliyezaliwa na Mungu hatendi dhambi, kwa sababu uzao wake wakaa ndani yake; wala hawezi kutenda dhambi kwa sababu amezaliwa kutokana na Mungu" (1Yohana 3:9)

Mungu anapotuangalia anatarajia kutuona tukiishi bila kuugua-ugua kwa kuwa imeandikwa, "Mwenyewe aliutwa udhaifu wetu, Na kuyachukua magonjwa yetu" (Mathayo 8:17); Na kwa kupigwa kwake tuliponywa (1Petro 2:24)

Bwana hafurahi anapowaona watu wake wanaishi kama omba-omba, duni na bila tumaini kwa kuwa imeandikwa "Na Mungu wangu atawajazeni kila mnachokihitaji kwa kadri ya utajiri wake, katika utukufu, ndani ya Kristo Yesu" (Wafilipi 4:19)

Bwana hafurahi anapowaona watu wake wakiwa katika hali ya unyonge na dhaifu, kwa kuwa imeandikwa, " kwa maana ndiye Mungu atendaye kazi ndani yenu, kutaka kwenu na kutenda kwenu, kwa kulitimiza kusudi lake jema" (Wafilipi 2:13).

Na pia imeandikwa;

"Aliye dhaifu na aseme, Mimi ni hodari" (Yoeli 3:10)

Bwana hafurahi anapowaona watu wake wanaishi katika hofu ya kumwogopa shetani na hila zake, wakati imeandikwa; "Tazama, nimewapa amri ya kukanyaga nyoka na nge, na nguvu zote za yule adui, wala hakuna kitu kitakachowadhuru." (Luka 10:19)

Na pia imeandikwa;

"Ninyi, watoto wadogo, mwatokana na Mungu; nanyi mmewashinda, kwa sababu yeye aliye ndani yenu ni mkuu kuliko yeye aliye katika dunia" (1Yohana 4:4)

Kwa nini ahadi hizi hazionekani zikitenda kazi kati ya watu wengi wa Mungu?
Na tujifunze toka kwenye safari ya wana wa Israeli. Ni kweli kwamba ingawa wana wa Israeli wote walitolewa kutoka Misri, lakini SI WOTE wale walioanza safari waliomaliza na kufika katika nchi ya ahadi.

Biblia inatuambia ya kuwa kati ya wale walioanza safari ni Yoshua na Kalebu tu ambao waliweza kufika katika nchi ya ahadi, na kuyafurahia matunda ya kukombolewa kwao.

Hivi leo wangekuwa hai katika mwili Yoshua na Kalebu, na kanisa liwaulize swali hili, "Je ni siri gani iliyowawezesha kufika Kanani wakati wenzenu walishindwa hata Musa pia?"

Jibu lao lingekuwa hili:

"Tuliweza kufika kanani na wenzetu wakashindwa kwa kuwa tulimfuata Bwana kwa kila neno". (Kumbukumbu la Torati 1:32-39)

Na hao wengine walishindwaje kuingia Kanani?

Biblia inajibu:

"Basi twaona ya kuwa hawakuweza kuingia kwa sababu ya kutokuamini kwao" (Waebrania 3:19). Maana hawakuwa watendaji wa Neno. Kutokuamini maana yake ni kutokuwa mtendaji wa Neno.

Hali hii ni sawa kabisa na hali ilivyo katika kanisa, kati ya watu wa Mungu. Wale wanaolifuata neno la Kristo na kulitenda, wanarithi ahadi za Mungu, na kuufurahia wokovu walioupata, tangu wakiwa hapa duniani.

Na wako watu wa Mungu wengi sana ambao hali zao kiroho na kimwili ni duni (wako jangwani) kwa sababu ya kutokuamini kwao.

Wamelitilia mashaka Neno la Kristo. Hawana uhakika kuwa lile ambalo Mungu ameahidi katika maandiko ni kweli.

Na kwa sababu hii wamedumaa kiroho, hawakui tena, na kwa sababu wengi wao ni viongozi katika kanisa, na kanisa nalo limedumaa.

Je! Bwana wetu atavumilia kuliona kanisa lake linazidi kuchakaa hata lini? Kumbuka jambo hili:

MUNGU SIKUZOTE NA WAKATI WOTE HUSEMA KILE ANACHOKIMAANISHA; NA ANAMAANISHA KILE ANACHOKISEMA.

SHETANI SIKUZOTE NA WAKATI WOTE HUSEMA MUNGU HAMAANISHI KILE ANACHOKISEMA; NA ANASEMA ASICHOKIMAANISHA.

Sasa ni uamuzi wako, kumsikiliza Mungu au kumsikiliza shetani.

"Lakini pasipo imani haiwezekani kumpendeza; kwa maana mtu amwendeaje Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko, na kwamba huwapa thawabu wale wamtafutao" (Waebrania 11:6)

Lakini kumbuka kuwa chanzo cha imani ni kulisikia na kulitenda neno la Kristo. Ahadi hizi zote hazionekani katika watu wa Mungu kwa sababu watu wamekuwa wasikiaji tu na wala si watendaji wa Neno.

Na tuzungumze na Yoshua juu ya kazi yake hiyo aliyopewa:

"Je! Yoshua uliwezaje kufanikiwa kuwafikisha wana wa Israeli katika nchi ya ahadi? Ulitumia mbinu gani katika kufanikisha wajibu huo?"

Yoshua angetuambia tusome kitabu cha Yoshua 1:8

"Kitabu hiki cha torati kisiondoke kinywani mwako, bali yatafakari maneno yake mchana na usiku, upate kuangalia kutenda sawasawa na maneno yote yaliyoandikwa humo; maana ndipo utakapoifanikisha njia yako, kisha ndipo utakapositawi sana".

Hizi ni mbinu ambazo Yoshua alipewa ili aweze kufanikiwa katika jukumu alilopewa.

Na kwa kuwa hili ni neno la Mungu ambalo linadumu milele, tukilifuata na tukilitenda sawasawa na Mungu alivyoagiza, na sisi tutafanikiwa na kusitawi kuanzia hapa duniani tukifanya kazi ya kuwa mabalozi wa Kristo.

Lazima tuanze kuchukua hatua za imani ambazo zitatufanya tukanyage nyayo zetu juu ya ahadi ambazo Mungu ametupa; nazo zitakuwa zetu.

Lakini kama vile wana wa Israeli walivyopigana vita ili kukanyaga nyayo zao juu ya nchi waliyoahidiwa, vivyo hivyo na sisi inatubidi tupigane vita vya imani ili tuweze kurithi ahadi tulizopewa.

Bwana alipokuwa anatuita katika utumishi, Roho wake alituongoza kuyatafakari maagizo aliyompa Yoshua, mwana wa Nuni.

Tuliposoma maneno haya; "kitabu hiki cha torati…..", mawazo yetu haraka yalifikiri kinazungumziwa kitabu cha kumbukumbu ya torati. Kwa hiyo tukakisoma kitabu chote cha kumbukumbu ya torati, lakini hatukuelewa kitu.

Ndipo Bwana akasema ndani ya roho zetu ya kuwa, Haikuandikwa kitabu hiki cha kumbukumbu ya torati, ingekuwa ni hivyo, basi ingeandikwa kitabu kile cha torati badala ya kitabu hiki cha torati.

Lakini pia kitabu hicho mnachosoma ni kitabu cha Yoshua, ingekuwa inamaanisha kitabu cha Yoshua, basi ingeandikwa kitabu hiki cha Yoshua, badala ya kitabu hiki cha torati.

Je, hamjasoma kwamba imeandikwa wapi, "msidhani ya kuwa nalikuja kutangua torati au manabii, la, si kuja kutangua bali kutimiliza"?

Tulipoutafuta mstari huu umeandikwa wapi, tuliukuta katika kitabu cha Mathayo 5:17.

Ndipo Roho wa Bwana akatuwezesha kuelewa kuwa "kitabu cha torati ……." Ina maana maagizo yote ya Mungu aliyopewa Musa. Na kwetu sisi ina maana agano la kale pamoja na agano jipya.

Na mambo ambayo tunatakiwa kuyafanya juu ya kitabu hiki cha torati (Neno la Mungu) ni haya:

Kisiondoke kinywani mwetu
Tuyatafakari maneno yake mchana na usiku,
Tupate kuangalia kutenda sawasawa na maneno yote yaliyoandikwa humo

Matokeo ya kuyafanya mambo haya ni kufanikiwa na kusitawi sana kiroho na kimwili kama Mungu alivyokusudia ndani ya Kristo.

Mbinu hizi zinatuwezesha kuwa watendaji wa Neno, na si wasikiaji tu hali tukijidanganya nafsi zetu. Hebu tuangalie mbinu mojawapo kati ya hizi na tuone jinsi zinavyooana na zingine na kuleta mafanikio katika maisha yetu ya kila siku


KUTAFAKARI NENO
"Kitabu hiki cha torati kisiondoke kinywani mwako, bali YATAFAKARI MANENO YAKE MCHANA NA USIKU, upate kuangalia kutenda sawasawa na maneno yote yaliyoandikwa humo; maana ndipo utakapoifanikisha njia yako, kisha ndipo utakapositawi sana". (Yoshua 1:8)

Mtu mmoja aliwahi kutuuliza swali hili: "Je, kutafakari maana yake nini?" Kila mara tunapofundisha somo hili tunakutana na swali la jinsi hii.

Tunaamini kuwa swali hili linawatatanisha wengi kwa sababu bado hawajatofautisha kati ya kusoma neno na kutafakari neno.

Kusoma neno ni tofauti na kutafakari neno. Kulitafakari neno ni zaidi ya kulisoma neno. Watu wengi huwa wanasoma neno zaidi kuliko kutafakari.

Kutafakari maana yake nini?

Maana ya karibu sana ya neno kutafakari ni kuwaza. Ni kusoma neno huku unalicheua na kulitafakari au kuliwaza rohoni mwako.

Kutafakari ni njia mojawapo kubwa ya kuweza kuilisha roho yako. Yesu Kristo alisema Imeandikwa, "mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu" (Mathayo 4:4)

Mkate ni chakula cha mwili wa nje wa nyama na damu; neno la Mungu ni chakula cha mwili wa kiroho. Kinywa kinapokea chakula na meno yanatafuna, na kukivunja huku kikilainishwa na mate, tayari kwa kumezwa.

Kusoma neno ni kama kinywa, kazi yake ni kulipokea neno. Kutafakari ni kuvunjavunja hilo neno huku Roho wa Mungu akililainisha liwe tayari kumezwa na roho yako.

Kutafakari neno kunamletea mtu siri ya ajabu ya uhakika na ushindi ndani ya Kristo.

Sisi ni watenda kazi pamoja na neno la Mungu hapa ulimwenguni. Tunaliwakilisha Neno la Kristo mahali tulipo na ulimwenguni pote.

Na kwa sababu hiyo, Imeandikwa, "Neno la Kristo na likae kwa wingi ndani yenu katika hekima yote" (Wakolosai 3:160

Huwezi ukawa na Neno la Kristo moyoni mwako bila ya kuitumia siri ya kutafakari. Kukariri neno la Kristo hukukuletei uhakika na ushindi kiroho na kimwili kama vile kutafakari kunavyofanya ndani ya mtu.
Kutafakari ni kuwaza.

Tatizo kubwa sana ambalo linawapata watu ni tatizo la mawazo. Na huu ni ugonjwa mkubwa sana ambao umewakwamisha wengi katika maisha yao ya kiroho.

Kutafakari na kuwaza ni jambo la rohoni, ni jambo la moyoni.

Mtu anapowaza, au kutafakari jambo huwa ni jambo linalofanyika moyoni mwake, ingawa utadhani linafanyika katika ubongo.

Je! wewe unayesoma somo hili sasa hivi unawaza nini moyoni mwako, unatafakari nini? Mara nyingi utaona mtu anaposoma mawazo yake (roho yake) yanakuwa mbali sana, kwa hiyo hakuna anachoelewa katika hayo anayosoma.

Pia, hata wakati watu wanasikiliza neno la Mungu, mara nyingi mawazo yao yanakuwa mbali sana na neno linalofundishwa. Hii inajidhihirisha hasa ukimuuliza ya baada muda mchache baadaye, juu ya neno lililofundishwa maana hatakumbuka.

Unapoumwa huwa unawaza nini? Wengi wanautafakari ugonjwa, na wengine hata kukata tamaa anapoona hauponi haraka. Wengine wanapoumwa wanawaza na kutafakari kufa kuliko kuishi.

Unapokuwa una matatizo huwa unawaza nini? Unapokosa maelewano na mwezako, nyumbani, kazini au mahali popote, huwa mawazo yako yanawaza nini?

Unapokuwa huna fedha au vitu fulani vya kimwili huwa unawaza au kutafakari nini?

Tunaweza kusema mengi, lakini swali kubwa ni hili’ "kila wakati huwa unawaza nini na kutafakari nini?"
Je! unafahamu ya kuwa matendo yako na maneno yako, ni matokeo ya mawazo uliyonayo? Mtu husema anachokitafakari au kukiwaza, na pia hutenda anachokitafakari au kukiwaza moyoni mwake.

Ukitaka kumfahamu mtu alivyo moyoni mwake, sikiliza maneno anayosema na angalia matendo anayoyatenda.

Hakuna katika biblia ambapo mtu wa Mungu ameambiwa haitafakari shida yake, awaze juu ya ugonjwa wake au udhaifu wake.
Kumbuka kuwa maneno ni chakula cha roho, hali ya roho yako inategemea sana ni maneno gani unayasikia kila wakati na kuyatafakari.

Unapotafakari maneno unailisha roho yako. Ukitafakari neno la Mungu roho yako inajengeka katika kumjua Mungu.

Ukitafakari shida, magonjwa, hofu, unaifanya roho yako ijengeke katika hayo.

Watu wengi sana wamejengeka katika kumwogopa shetani kuliko Mungu. Hii hali ipo hata kwa watu wa Mungu. Hayo ni matokeo ya kumtafakari shetani na majaribu anayowajaribu, kuliko kumtafakari Mungu na uweza wake.

Neno la Kristo linakosa nafasi katika mioyo ya watu, kwa sababu mioyo ya watu imejaa mawazo ya dunia hii na shida zake. Mioyo ya watu imejaa mawazo yanayopinga na kwenda kinyume kabisa na neno la Kristo.

Moyo wa mtu ni uwanja wa vita. Ukishinda vita katika mawazo, utakuwa umeshinda vita katika mwili, katika roho na katika maneno.

Je umewahi kujiuliza kwa nini Nabii Ezekieli aliambiwa ale gombo la chuo, na Yohana aliambiwa ale kitabu kilichofunguliwa.

Kwa nini hawa kuambiwa kusoma tu ambayo yalikuwa yameandikwa bila kula gombo la chuo na kitabu kilichofunguliwa?

Nini tofauti ya kusoma na kula. Kunatofauti kubwa kati ya kusoma ujumbe wa Mungu na kula ujumbe wa Mungu.

Soma Ezekeili 2:7-10; 3:1-3 na Ufunuo wa Yohana 10:1,2, 8-11.

Mtu anapokula chakula, huwa kinatafunwa na kulainishwa kabla ya kumezwa. Na kikimezwa na kuingia tumboni, kinanyonywa na kuingia katika mishipa ya damu inayozunguka mwili mzima kukisambaza chakula hicho katika sehemu zinazohitajika.

Mtu anapotembea, ukweli ni kwamba ni chakula kile alichokula ndicho kinachotembea, INGAWA yeye ndiye anayeonekana anatembea.

Kwa hiyo Ezekieli na Yohana walipokula ujumbe wa Bwana uliokuwa umeandikwa katika gombo la chuo na katika kitabu kilichofunuliwa, ujumbe huo uliingia ndani yao kama vile ambavyo wangekula nyama.

Ujumbe huo iliingia kwenye damu yao na ukajenga misuli. Kila sehemu ili kuwa imejaa ujumbe wa Mungu. Ujumbe huo ndiyo uliowafanya wapate nguvu ya kutembea, na kuishi, na kusema.

Kwa mtazamo mwingine tunaweza kusema, Ezekieli na Yohana walikuwa ni ujumbe wa Mungu uliokuwa unatembea.

Na sisi tukilitafakari neno la Kristo, na likijaa ndani yetu kwa wingi, tunakuwa ni neno la Kristo linalotembea; tunakuwa ni neno la Kristo, linalosema; tunakuwa ni neno la Kristo

linaloponya; tunakuwa neno la Kristo linaloshauri; tunakuwa Nuru ya Mungu kwa wengine!

Tunafika mahali ambapo kuishi kwetu kunakuwa ni neno (Kristo) – kama vile Paulo alivyosema "kuishi ni Kristo" (Wafilipi 1:21)

Mtu anashindwa kuwa mtendaji wa Neno kwa kuwa moyoni mwake hakuna neno. Anabaki kuwa mtendaji wa maneno mengine aliyonayo mawazoni mwake tu.

"Maana ingawa tunaenenda katika mwili, hatufanyi vita kwa jinsi ya mwili; (maana silaha za vita vyetu si za mwili, bali zina uwezo katika Mungu hata kuangusha ngome;) tukiangusha MAWAZO na kila kitu kilichoinuka, kijiinuacho juu ya elimu ya Mungu; na tukiteka nyara KILA FIKRA ipate kumtii Kristo" (2 Wakoritho 10:3-5) Hii ina maana kuwa fikra zako ziwaze sambasamba na Neno (Kristo).

Katika kuishi kwetu na kuenenda kwetu tuwe tunatafakari nini mioyoni mwetu, ili roho zetu zipate chakula safi cha kiroho?

"Hatimaye, ndugu zangu, mambo yoyote yaliyo ya kweli, yoyote yaliyo ya staha, yoyote yaliyo ya haki, yoyote yaliyo safi, yoyote yenye kupendeza, yoyote yenye sifa njema; ukiwapo wema wowote, ikiwapo sifa nzuri yoyote, YATAFAKARINI HAYO" (Wafilipi 4:8)

Mambo yote haya yaliyotajwa utayakuta katika neno la Mungu. Kwa kutafakari neno la Kristo usiku na mchana katika mambo yote ndipo utakapoifanikisha njia yako ya wokovu na ndipo utakapositawi sana kiroho na kimwili.

Na biblia inasema mtu anayelitafakari neno la Mungu usiku na mchana; anakuwa mtu wa namna hii:
"KILA ALITENDALO LITAFANIKIWA" (Zaburi 1:3)

Fanya hivyo na wewe utafanikiwa.

Unapoumwa usitafakari ugonjwa, wala kuwaza maumivu yake, bali tafakari neno la Mungu juu ya uponyaji nalo litakuwa afya mwilini mwako. Maana imeandikwa hivi:

"Mwanangu, sikiliza maneno yangu; Tega sikio lako, uzisikie kauli zangu. Zisiondoke machoni pako; Uzihifadhi NDANI YA MOYO WAKO. Maana ni uhai kwa wale wazipatao, Na AFYA ya mwili wao wote." (Mithali 4:20-22)

Unapolitafakari neno la Mungu ndipo unapolihifadhi neno hilo ndani ya moyo wako. Na neno la Mungu likihifadhiwa ndani ya moyo wako linakuwa AFYA mwilini mwako, na magonjwa hayatakusumbua tena.

Ukilihifadhi neno la Mungu lenye nguvu za uponyaji ndani ya moyo wako utajua hakika kwamba kwa kupigwa kwake (Yesu Kristo) sisi tumepona". (Isaya 53:5)

Wengi wanapata matatizo katika kupokea uponyaji kwa sababu wanaamini kuwa Mungu atawaponya siku moja akipenda kwa sababu wameomba au wameombewa. Hili ni tumaini na siyo imani. Tumaini siku zote muda wake ni baadaye na imani siku zote muda wake ni sasa.

Imani ya uponyaji huja kwa kusikia na kutenda neno la Mungu linalozungumzia uponyaji. Neno linatuambia ya kuwa tulipona siku nyingi zilizopita kwa kupigwa kwake Yesu Kristo na SIYO tutapona siku moja. Unapompokea Kristo moyoni mwako, magonjwa yanakuwa hayana tena mamlaka juu yako.

Na ili uwe na uhakika wa afya ya mwili wako kila wakati, inakubidi uwe na tabia ya kulihifadhi neno la Kristo moyoni kwa kulitafakari.

Siku moja mtu mmoja aliyekuwa anaumwa alituambia kwa huzuni; "Mimi nimeombewa kwenye mkutano wa injili lakini bado sijapona, ingawa niliwaona wenzangu wengi wakisimama kushuhudia kuwa wamepona".

Tukamwambia; "Na wewe umepona lakini tatizo lako ni kwamba hujui ya kuwa umepona"

Akauliza kwa mshangao; " Inawezekana wapi mtu asijijue ya kuwa amepona na huku bado maumivu anayo hata baada ya maombezi?"

Roho wa Mungu akatuonyesha kwa undani zaidi kwa nini mtu huyo alishindwa kupokea uponyaji.

Tukamwambia; "Uponyaji huwa unapokelewa kwanza katika roho na ndipo unajidhihirisha katika mwili. Wewe ulitaka kwanza uone maumivu yamekwisha, ndipo uamini moyoni mwako ya kwamba umepona. Unatakiwa uwe na uhakika kuwa umepona kwa sababu neno la Mungu linasema umepona na siyo mwili unasemaje"

Mtu huyu alikuwa na tatizo ambalo watu wengi wanalo. Ni tatizo la kukosa uhakika unaodumu wa kuhusu roho zao na miili yao.

Neno la Mungu ndilo kweli inayodumu milele. Neno la Mungu ndilo linalompa mtu uhakika wa jambo ambao hauwezi kuyumbishwa na kitu chochote.

Neno la Mungu linahifadhiwa ndani ya moyo wa mtu kwa kulitafakari na siyo kwa kukariri. Mtu anayekariri mistari ya biblia ni sawa sawa na mtu anayekula mahindi au chakula chochote bila kutafuna.
Neno la Kristo na likae moyoni mwako kwa uwingi katika hekima yote (Wakolosai 3:16).

Kumbuka, Neno la Mungu moyoni mwako ndilo linalokupa uhakika wa mambo yako yote; (wokovu, uponyaji, ushindi katika majaribu, mamlaka yako juu ya shetani na kazi zake, uzima wa milele, na kadhalika.)

Na huo ndio msingi mkubwa wa imani, kwa kuwa "imani ni kuwa na hakika ya mambo….." (Waebrania 11:1).

Kabla imani yako katika Kristo haijaonekana katika matendo yako na maneno yako, ni lazima ijengeke kwanza katika moyo wako kwa njia ya kulitafakari au kuliwaza neno la Mungu katika mambo yako yote.

Matokeo yake ni kwamba utakuwa na uhakika wa jambo lolote moyoni mwako na kwa ajili hiyo utakuwa na ujasiri wa kulisema na kulitenda.

Usipokuwa na uhakika wa jambo moyoni mwako, huwezi ukawa na ujasiri wa kulisema na kulitenda.

Neno la Mungu ndilo nuru na taa miguuni petu sisi tulio ndani yake (Zaburi 119:105); na kwa sababu hiyo tunaishi katika imani iliyo na uhakika udumuo, na wala si wa kubahatisha.

Je, umewahi kuutafakari mstari huu ufuatao:

"Kila mtu aliyezaliwa na Mungu hatendi dhambi, kwa sababu uzao wake wakaa ndani yake; wala hawezi kutenda dhambi, kwa sababu amezaliwa kutokana na Mungu" (1Yohana 3:9)

Swali kubwa tulilojiuliza kwa siku nyingi mpaka Bwana alipotusaidia, lilikuwa, ninawezaje kuishi hapa duniani na tusiweze kutenda dhambi?

Tunaamini hili ni swali ambalo wengi linawasumbua; na hata ambao si wakristo au hawajaokoka wanajiuliza swali.

Mstari huu unatupa maana ya kwamba mtu yeyote aliyezaliwa na Mungu mara ya pili kwa uweza wa neno lake (1Petro 1:23), anatakiwa aishi kuanzia hapa duniani katika utakatifu kama vile Baba yake (Mungu) alivyo mtakatifu, WALA ASITENDE DHAMBI!

Unaweza ukajiuliza na hata kukataa kuwa hii haiwezekani. Lakini kabla ya kukataa naomba ujibu swali hili; "Unadhani Mungu ni dhalimu kiasi hicho kukwambia ufanye jambo ambalo anajua huna uwezo wa kufanya?"

Mungu si dhalimu, maagizo yote aliyotupa, ametupa pia na njia ya kuyafanya.

Kwa hiyo unaweza ukaishi katika utakatifu bila kutenda dhambi!

Imeandikwa:

"Moyoni mwangu nimeliweka neno lako, NISIJE NIKAKUTENDA DHAMBI" (Zaburi 119:11)

Ukiliweka neno la Mungu moyoni mwako kwa kulitafakari, unaweza ukaishi bila kutenda dhambi, kwa kuwa neno hilo litakuwa nuru na taa miguuni pako (Zaburi 119:105)

Unaanguka mara kwa mara katika dhambi kwa kuwa HUNA NENO LA KRISTO KWA UWINGI MOYONI MWAKO; na kwa sababu hiyo unashindwa kuwa mtendaji wa Neno.
Anza sasa kuwa na tabia ya kulitafakari au kuliwaza neno la Mungu usiku na mchana, utakuwa na akiba ya kutosha ya kukufanikisha wewe na wenzako.

Neno la Mungu ndicho chakula cha roho yako. Lisha roho yako kwa Neno la Mungu kama vile ambavyo unaulisha mwili wako chakula kinachotoka kwenye udongo.

Yesu Kristo ndiye chakula cha uzima kilichoshuka toka mbinguni. Unapomtafakari Kristo, unaifanya sura yake na tabia yake viumbike moyoni mwako.

"Mimi ndimi chakula chenye uzima kilichoshuka kutoka mbinguni; mtu akila chakula hiki, ataishi milele. Na chakula nitakachotoa mimi ni mwili wangu, kwa ajili ya uzima wa ulimwengu" (Yohana 6:51)

Kumtafakari Kristo (Neno) ni kula na kutafuna na kumeza chakula cha uzima. Na chakula hiki (Kristo) kinatufanya tuwe wazima kiroho na kimwili.

"Kwa hiyo, ndugu watakatifu, wenye kuushiriki mwito wa mbinguni, MTAFAKARINI SANA Mtume na Kuhani Mkuu wa maungamo yetu, Yesu" (Waebrania 3:1)

Kuna habari ya kweli ambayo ilitokea katika mji mmoja hapa Tanzania, itakayokupa picha ya umuhimu wa kulitafakari neno ili kula chakula cha kiroho.

Kuna mtu mmoja tajiri sana kwa mali ya dunia hii. Ana fedha za kutosha, ana magari mengi ya kwake binafsi, ana nyumba zake, na mali nyingine nyingi.

Siku moja alianguka chini ghafla na kuzimia. Basi, rafiki zake walimbeba haraka sana na kumpeleka hospitalini. Alipofika hospitalini huku bado amezimia, madaktari walimpima kwa vipimo vingi bila kufanikiwa kuona kilichomfanya aanguke na kuzimia.

Na walipokuwa wanachunguza zaidi jambo hili waliona kuwa mtu huyo tajiri alikuwa na tatizo la kutokula chakula vizuri. Kwa hiyo wakamwekea "drip’ ya maji ya "glucose" (maji yenye sukari).

Mara baada ya kumwekea hiyo "drip" aliamka na akashangaa alipojikuta yuko hospitalini na madaktari wamemzunguka. Alipewa chakula zaidi, akapata nguvu na akarudi nyumbani akiwa mzima bila kupewa dawa yoyote ila chakula tu.

Tatizo la mtu huyo ni kwamba ingawa alikuwa na kila kitu cha kumwezesha kupata chakula, alikuwa hana muda wa kukaa chini na kula chakula. Kila wakati alikuwa ni mtu wa shughuli nyingi.

Tulipoambiwa habari hii, Roho wa Mungu alitukumbusha hali ya watu wa Mungu wengi walivyo hivi sasa. Wamezimia kiroho, moto wa injili na maombi umepoa ndani yao kwa sababu hawana nafasi ya kukaa chini na kula chakula cha kiroho.

Kwa sababu wana shughuli nyingi, hawapati kabisa wakati wa kula neno la Mungu kwa kutafakari. Matokeo yake ni kuzimia kiroho. Wakipewa "drip" ya maombi wanasimama na kuendelea kiroho. Lakini kuendelea huku hakudumu kama hawapati nafasi ya kutulia mbele za Mungu na kulitafakari Neno lake – wao wenyewe binafsi.


Kwa hiyo hatua ya kwanza katika kuwa mtendaji wa Neno ni KULITAFAKARI NENO LA MUNGU USIKU NA MCHANA.

Hii ni muhimu sana kwa kuwa katika Kristo (Neno) tunaishi, tunakwenda, na tunakuwa na uhai wetu.

"Kwa maana ndani yake yeye (Kristo au Neno) tunaishi, tunakwenda, na kuwa na uhai wetu" (Matendo 17:28).


Source: mwakasege.org
Axact

Axact

Vestibulum bibendum felis sit amet dolor auctor molestie. In dignissim eget nibh id dapibus. Fusce et suscipit orci. Aliquam sit amet urna lorem. Duis eu imperdiet nunc, non imperdiet libero.

Post A Comment:

0 comments: